VIKUNDI 26 VYA WANAWAKE, VIJANA NA WATU WENYE ULEMAVU VYAPATIWA MIKOPO YA ASILIMIA 10 LONGIDO
















NA ABRAHAM NTAMBARA, LONGIDO

Halmashauri ya Wilaya ya Longido leo, Desemba 11, 2025, imetoa mikopo ya asilimia 10 yenye thamani ya shilingi 150,000,000 kwa jumla ya vikundi 26 vya Wanawake, Vijana na Watu Wenye Ulemavu.

Akizungumza katika hafla ya utoaji wa mikopo hiyo iliyofanyika kwenye Ukumbi wa J.K Nyerere, Mkuu wa Wilaya ya Longido Mhe. Kalli ameeleza mgawanyo wa mikopo hiyo kama ifuatavyo: Wanawake–Vikundi 11, shilingi milioni 60, Vijana–Vikundi 10, shilingi milioni 62 na Watu Wenye Ulemavu–Vikundi 5, shilingi milioni 28

Mhe. Kalli amevitaka vikundi hivyo kutumia mikopo hiyo kwa malengo yaliyokusudiwa ili kujiendeleza kiuchumi na siyo kwa matumizi ya starehe.

“Haya yanayofanyika leo ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa Halmashauri zote nchini kukusanya na kutenga asilimia 10 ya mapato ya ndani kwa ajili ya mikopo kwa vikundi vya Wanawake, Vijana na Makundi Maalum,” amesema Mhe. Kalli na kuongeza,

“Baada ya kupata fedha hizi, nendeni mkazitumie kwenye malengo yenu ili zizae, mrejeshe na wengine wapate. Tunaamini mtazitumia vizuri na tutajionea matokeo.”

Amefafanua kuwa mikopo hiyo ni ya awamu ya kwanza kwa mwaka wa fedha 2025/2026, na kurejeshwa kwake kutasaidia kutoa mikopo kwa vikundi vingine. Aliwataka wanufaika kuwa waaminifu na kurejesha mikopo kwa wakati bila kufuatiliwa.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Longido Mhe. Thomas Ngobei amesema mikopo hiyo imetokana na ukusanyaji wa mapato ya ndani ya Halmashauri. Ameahidi kuendelea kusimamia ukusanyaji wa mapato ili kuongeza kiwango cha mikopo kitakachotolewa katika awamu zinazofuata.

Ameongeza kuwa vikundi vilivyopata mikopo siyo kwamba ndivyo pekee vilivyoomba, na amevitaka kuwa mabalozi wa kuhamasisha vikundi vingine kuendelea kuomba na kuwa na imani na Halmashauri.

Naye Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Mhe. Peter Lekanet amewahimiza wanufaika kutumia fedha hizo kwa umakini na kuonesha matokeo chanya ili Serikali iendelee kutenga fedha zaidi kwa ajili ya mikopo ya wananchi.

Aidha, Afisa Maendeleo ya Jamii wa Wilaya ya Longido Bi. Grace Mghase amesema kuwa kupitia mfumo mpya wa utoaji mikopo ulioanzishwa na Halmashauri kwa mwaka wa fedha 2024/2025, jumla ya shilingi 396,000,000 ilitolewa kwa vikundi 43 vya Wanawake, Vijana na Watu Wenye Ulemavu.

Kwa mwaka huu wa fedha 2025/2026, Halmashauri imetoa shilingi 150,000,000 kwa vikundi 26, hivyo kufanya jumla ya mikopo iliyotolewa kwa kipindi cha 2024/2025 hadi 2025/2026 kufikia shilingi 546,000,000.

Bi. Mghase ameongeza kuwa vikundi vilivyonufaika vimekidhi vigezo baada ya kufanyiwa tathmini na Kamati ya Mikopo ya Halmashauri, kupitishwa na Timu ya Uendeshaji, na baadaye kuhakikiwa na Kamati ya Uhakiki ya Wilaya.

Post a Comment

0 Comments