NA ABRAHAM
NTAMBARA, LONGID
Mkuu wa Wilaya ya
Longido, Mhe. Salum Kalli, ametoa siku 12 kwa vikundi vinavyodaiwa mikopo ya
asilimia 10 ya Halmashauri vilivyokopa kuanzia mwaka 2017 hadi 2022 kuhakikisha
vinarejesha mikopo hiyo.
Kauli hiyo ameitoa
leo Januari 19, 2026, wakati akizungumza na vikundi hivyo katika ukumbi wa
Halmashauri wa JK Nyerere, ambapo amesema muda huo utaisha Januari 31, 2026.
Mhe. Kalli amesema
kuanzia Februari 1, 2026, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya kwa
kushirikiana na Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii watapita kikundi kwa
kikundi kuhakiki kiasi kilichokopwa na kilichorejeshwa.
Amesisitiza kuwa
vikundi ambavyo havitakuwa vimerejesha mikopo hiyo vitachukuliwa hatua kali za
kisheria.
“Lengo la
kuwakopesha ni kuwasaidia mfanye maendeleo yenu, lakini ni lazima mrejeshe ili
na wengine wapate. Mikopo hii inasaidia wananchi kuepuka mikopo ya kausha damu.
Sasa kama mnakopeshwa na hamrejeshi, wengine watakopeshwa nini?” amesema Mhe.
Kalli.
Hata hivyo, Mhe.
Kalli amevitaka vikundi hivyo kutumia mikopo waliyopewa kwa malengo
yaliyokusudiwa badala ya kugawana fedha hizo kwa matumizi binafsi yasiyohusiana
na shughuli za kikundi, jambo ambalo limekuwa chanzo cha kushindwa kurejesha
mikopo kwa wakati.
Katika hatua
nyingine, Mhe. Kalli amemuagiza Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya
Wilaya ya Longido kuwaandikia barua Watendaji wa Kata ili kuwapa maelekezo ya
kuwafahamisha Waheshimiwa Madiwani kuwa wao wasiwe sababu ya vikundi
vilivyokopeshwa kuacha kurejesha mikopo hiyo kwa wakati.
Kwa upande wake,
Katibu Tawala wa Halmashauri hiyo, Bi. Rahma Kondo, amesema hakuna kikundi
kitakachosamehewa kurejesha mikopo hiyo, na kuvitaka vikundi kuacha kutoa
visingizio vya kushindwa kurejesha mikopo kwa madai ya ukame, akieleza kuwa
baadhi ya vikundi vilikopa wakati hakukuwa na ukame.
Amebainisha kuwa
kuna vikundi vinavyoendesha biashara kubwa na zinazoonekana wazi, lakini kwa
makusudi vinashindwa kurejesha mikopo hiyo. Pia amewataka watumishi wa umma
waliokopa kurejesha mikopo yao kwa kuwa orodha yao ipo.
Mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri haina riba na hutolewa kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kwa lengo la kuwawezesha kiuchumi.
0 Comments