DC LONGIDO AWATAKA WATUMISHI WA AFYA KUWA NA LUGHA YA STAHA KWA WAGONJWA






NA ABRAHAM NTAMBARA, LONGIDO

Mkuu wa Wilaya ya Longido, Mhe. Salum Kalli, amewataka watumishi wa sekta ya afya wilayani humo kuwa na lugha ya staha na kuwahudumia wagonjwa kwa heshima na upendo wanapotoa huduma za afya.

DC Kalli ametoa kauli hiyo leo Januari 9, 2026, alipokuwa akizungumza na wananchi wa Kata ya Namanga baada ya kupokea malalamiko yao kuhusu baadhi ya watumishi wa afya kutokuwa na lugha nzuri wanapowahudumia wagonjwa.

Kauli hiyo imetolewa katika mwendelezo wa ziara yake ya Kata kwa Kata yenye lengo la kusikiliza na kutatua kero za wananchi, sambamba na kuwahamasisha kujiunga na Bima ya Afya kwa Wote.

“Kuanzia leo, mtumishi wa afya anayeshindwa kuwahudumia wananchi ipasavyo aandike barua ya kuacha kazi. Mtumishi yeyote mwenye lugha chafu hatumtaki,” amesema DC Kalli.

Mhe. Kalli ametoa rai kwa watumishi wa afya kuhakikisha wanawahudumia wananchi kwa upendo na weledi, huku akisisitiza kuwa vituo vyote vya kutolea huduma za afya wilayani Longido vinapaswa kufanya kazi kwa masaa 24, na wagonjwa wasikose huduma kutokana na watumishi kutokuwepo vituoni.

Aidha, ametumia fursa hiyo kumwagiza Mganga Mkuu wa Wilaya ya Longido, Dkt. Mathew Majani, kuhakikisha anawafikishia maelekezo hayo watumishi wote wa afya wilayani humo.

Kwa upande wake, Mganga Mkuu wa Wilaya, Dkt. Majani, amepokea malalamiko hayo na kuahidi kuyafanyia kazi ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na zenye ubora wanaostahili.

Katika hatua nyingine, DC Kalli amesema Serikali inaendelea kufanya jitihada kubwa kutatua changamoto ya upungufu wa maji katika Kata ya Namanga.

Ameeleza kuwa mradi mkubwa wa maji wa Sinya unaendelea kutekelezwa na mkandarasi, na kwamba ndani ya miezi minne mradi huo unatarajiwa kukamilika.

Amesisitiza kuwa kukamilika kwa mradi huo kutaiwezesha Namanga kupata maji ya kutosha na ya uhakika kwa matumizi ya wananchi.

Post a Comment

0 Comments