Eng. Samamba: Kila Siku ni Nafasi ya Kuifanya Tanzania kuwa Kitovu cha Uongezaji Thamani wa Madini Barani Afrika




Mtumba, Dodoma

Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Eng. Yahya Samamba, amesema kuwa kila siku ni fursa mpya ya kuisukuma Tanzania mbele katika ajenda ya uongezaji thamani wa madini na kuimarisha nafasi yake kama kitovu cha uongezaji thamani wa madini barani Afrika.

Eng. Samamba ameyasema hayo leo, Februari 5, 2026, ofisini kwake Mtumba, wakati akizungumza na watumishi wa Wizara ya Madini waliompongeza kuadhimisha siku yake ya kuzaliwa. Katika mazungumzo hayo, amesisitiza kuwa umoja na mshikamano unaooneshwa na watumishi ni ishara ya ushirikiano imara unaohitajika kufanikisha malengo ya sekta.

Ameeleza kuwa Tanzania ina rasilimali nyingi, soko linalokua, na mazingira wezeshi ya uwekezaji, hivyo ni wajibu wa kila mdau wa sekta kutumia fursa hizo kuongeza thamani ya madini, kukuza ajira, na kuongeza mapato ya Serikali.

Aidha, Eng. Samamba ameongeza kuwa Wizara itaendelea kuimarisha mifumo ya usimamizi, kuhimiza uwekezaji kwenye teknolojia za uchakataji wa madini, na kusukuma mbele ajenda ya Madini Vision 2030; Madini ni Maisha na Utajiri, ili sekta ya madini iendelee kuwa chachu ya maendeleo ya viwanda na uchumi jumuishi nchini.

Akisisitiza dhamira hiyo, amesema: “Sote tuliopo hapa tumebarikiwa kwa uwepo, afya na uzima. Kila siku ni nafasi ya kufanya zaidi kutimiza lengo la uwepo wetu hapa duniani. Kwa sisi tuliopo katika Sekta ya Madini, kila siku ni fursa ya kuisukuma sekta hii kufikia malengo ya kitaifa. Mwelekeo wa sekta kwa sasa ni kuongeza thamani ya madini ndani ya nchi na kuuza bidhaa za mwisho, kujenga uwezo, na kuharakisha maendeleo kwa Taifa, jamii na vizazi vijavyo.”

Post a Comment

0 Comments