Mwandishi Wetu, Zanzibar
Chama Cha Mapinduzi ( CCM) kimesema wakati ifikapo Februari 5 Mwaka huu kitafikisha Miaka 49 toka kuzaliwa kwake Mwaka 1977, kinajivunia juhudi za kufikia shabaha na malengo ya kuundwa kwa chama hicho .
Vile vile CCM kimesisitiza kitaendelea kusimamia misingi ya Sera zake kwa kuendelea kuhubiri tija na faida ya ustawi wa Amani ,Umoja na Mshikamano wa kitaifa .
Katibu wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar, Idara ya Itikadi ,Uenezi na Mafunzo, Khamis Mbeto Khamis ameeleza hayo akiwa Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui .
Mbeto alisema kwa Miaka 49 Serikali za CCM zimemfanya Mtanzania atoke katika kadhia ya unyonge wa kunyonywa, kunyanyaswa na kudharauliwa hadi kuwa mtu huru anayeheshimika.
Alisema CCM katika kuamini Umoja wa Afrika, kimeshiriki kikamilifu katika harakati zilizoleta Ukombozi wa Mataifa mengine Kusini mwa Afrika na sasa yako huru.
"Kwa miaka 49 Sera za CCM zimemuweka mbali Mtanzania na maadui Ujinga,Umasikini na Maradhi. Tunaelewa maadui hao ni kazi kumalizika kwa pamoja .Mapambano dhidi yao yataendelea" Alisema Mbeto
Aidha alisema umadhubuti wa CCM utabaki katika kuziunganisha jamii , kufuta aina zote za unyonyaji, maonevu au jaribio lolote la kudhoofisha uchumi na kuzorotesha Maendeleo .
"Kuwepo kwa Vituo vya Afya, Zahanati na Hospitali ni kumkabili adui Maradhi. Kujenga Shule za Msingi na Vyuo Vikuu ni mkakati wa kufuta Ujinga. Miradi ya Kilimo ,Uvuvi, Ufugaji, ujenzi wa Viwanda, Barabara na Masoko ni kumfanya kila mtu ajijenge kiuchumi" Alisema Mbeto
Akizungumzia ustawi wa maendeleo ya demokrasia ndani ya CCM, Mbeto alisema ushiriki wa wanachama katika kuamua ,kuchagua na kuchaguliwa ,ni kielelezo cha kukomaa kwa tasisis hiyo.
'Kwa miaka 49 tumejenga taasisi imara, makini inayoaminiwa na kutegemewa na Wananchi wote. Pia Sera na Miongozo ya chama chetu imekuwa ikibadilka kulingana na mahitaji ya nyakati" Alieleza

0 Comments