NA MWANDISHI WETU
Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii katika Maonesho ya 50
ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) limeendelea kuvutia maelfu
ya wananchi kupitia matangazo ya moja kwa moja yanayoonesha vivutio vya utalii
vya Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro.
Kupitia runinga kubwa iliyofungwa katika banda hilo, wageni
wanapata fursa ya kushuhudia maajabu ya Kreta ya Ngorongoro, makundi ya wanyama
mbalimbali wakiwemo pundamilia, nyumbu, swala, nyati, pamoja na wanyama adimu
kama faru, simba, tembo na chui, hali inayowafanya wajisikie kana kwamba wapo
ndani ya hifadhi hiyo.
Afisa Uhusiano Mkuu wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, Bw.
Walter Mairo, amesema kuwa teknolojia hiyo inawawezesha wageni kufuatilia
matukio mbalimbali yanayotokea ndani ya hifadhi, ikiwemo maisha ya wanyama
katika Kreta ya Ngorongoro na tambarare za Ndutu, ambako hushuhudiwa mzunguko
wa maisha ya nyumbu kuanzia kuzaliwa, kukua, kuhama na kurejea kila mwaka kwa
ajili ya kuanzisha kizazi kipya.
Ameongeza kuwa matangazo hayo ya mubashara yanaonesha jinsi
teknolojia ya kidijitali na utalii wa asili vinavyoweza kushirikiana katika
kuelimisha, kuburudisha na kuitangaza Ngorongoro duniani. Amesema Ngorongoro si
hifadhi ya wanyamapori pekee, bali ni jukwaa la kimataifa linalounganisha
urithi wa asili, biashara na teknolojia katika eneo moja.
Wananchi wanakaribishwa kutembelea banda la Wizara ya
Maliasili na Utalii katika Maonesho ya Sabasaba ili kujionea vivutio hivyo na
kupata simulizi mbalimbali kuhusu Ngorongoro. Timu ya wataalamu wa hifadhi hiyo
ipo tayari kuwapa wageni taarifa na uzoefu unaoonesha kuwa Ngorongoro si mahali
pa kutazama vivutio pekee, bali ni mahali pa kujifunza, kuelewa na kuishi
uzoefu wa kipekee usiosahaulika.


0 Comments