WATUHUMIWA 17 MBARONI KWA KUUZA JEZI BANDIA ZA YANGA

Kamanda wa Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam ACP Muliro Muliro akiwaonyesha waandishi wa habari jezi bandia za timu ya Yanga Afrika 1208 ambazo wamezibaini zinazotengenezwa na kusambazwa na kampuni ya GSM. NA ABRAHAM NTAMBARA JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam linawashikilia watu 17 kwa tuhuma za kuuza jezi bandia za timu ya Yanga Afrika 1208 zinazotengenezwa na kusambazwa na kampuni ya GSM. Akizungumza na waandishi wa habari Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam ACP Muliro Muliro amesema kazi ya kuwakamata ilifanyika katika maeneo mbali mbali ya Jiji la Dar es Salaam, lakini pia kwa kushirikiana na baadhi ya mikoa nchini kwa kipindi cha kuanzia Januari 2 hadi Januari 28 mwaka huu. “Katika Jiji la Dar es Salaam Jeshi la Polisi limewakamata watuhumiwa watano, akiwemo Zahiri Hassan (17) Mmwera aliyekutwa huko Uwanja Benjamin William Mkapa akiwa na Jezi bandia za Timu ya Yanga 52, Kariakoo mtaa wa Agrey alikamatwa Majiba Ndahya (50) Msukuma akiwa na Jezi 124, Mohamed Ramadhani (26) Mchaga alikutwa na Jezi 86, John Staslaus (19) Mchaga alikamatwa na Jezi 39 na Emmanuel Kinasa (21) Msukuma alikutwa na Jezi 60,” Amesema ACP Muliro. Kamanda Muliro amesema watuhumiwa hao waliwataja wenzao wa Zanzibar, ambapo Uwanja wa Amani watuhumiwa watatu walikutwa na Jezi bandia 36. Ameeleza kuwa Jezi zingine bandia 134 zilipatikana kwa kushirikiana na Polisi Mkoa wa Tanga na Mwanza ambapo watuhumiwa tisa walikutwa na Jezi 811. “Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es salaam linawatahadharisha wananchi wote wanaojihusisha na vitendo vya kutengeneza, kuuza na kusambaza, bidhaa kwa kuiga au kufananisha nembo za biashara au huduma za watu wengine iliyosajiliwa kisheria, kufanya hivyo ni kosa na kinyume na sheria za nchi,” amesema na kuongeza,. “Jeshi la Polisi litashirikiana na mamlaka nyingine za kisheria ili kuona watuhumiwa wamechukuliwa hatua kali za kisheria,”.

Post a Comment

0 Comments