RAIS DKT. SAMIA KUFUNGUA MKUTANO WA KWANZA WA KITAIFA WA DIRA YA MAENDELEO YA TAIFA, lengo la mkutano ni kuzindua, kupokea na kujadili taarifa ya kitafiti….


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan.

NA ABRAHAM NTAMBARA

RAIS Dkt. Samia Suluhu Hassan atafungua Mkutano wa Kwanza wa Kitaifa wa Dira ya Maendeleo ya Taifa utakaofanyika Disemba 9, 2023 katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC) Jijini Dar es Salaam.

Hayo yamebainishwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji Prof. Kitila Mkumbo akizungumza na waandishi wa Habari Disemba 1, 2023 Jijini Dar es Salaam.

“Lengo kuu la Mkutano huu ni kuzindua, kupokea na kujadili taarifa ya kitafiti ya Tathimini ya Utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025,” amesema Prof. Mkumbo.

Prof. Mkumbo ameeleza kuwa Taarifa ya Kitafiti ya Tathimini ya Utekelezaji wa Dira ya Maendeleo 2025, pamoja na mambo mengine, imeainisha mafanikio yaliyopatikana na Changamoto zilizojitokeza katika utekelezaji wa Dira ya Kwanza ya Taifa ya Maendeleo.

Amesema Dira hii ilianza kutekelezwa Mwaka 2000 na itafikia mwisho wake mwaka 2025.

Kwamba pamoja na mafanikio mengine, taarifa ya tathimini inaonyesha kuwa pato la Taifa la Mtanzania (GDP per capital income) limeongezeka kutoka dola za kimarekani 399.5 (TZS 322,597) mwaka 2000 hadi Kufikia dola za kimarekani 1,200 (TZS 2,880,000) Mwaka 2022.

Prof. Mkumbo amebainisha kuwa Tanzania imefikia salimia 124 ya kujitolea kwa chakula ikilinganishwa na lengo la Kufikia asilimia 140 ifikapo 2025.

“Hatua hii imeiwezesha Tanzania kukabiliana na njaa kwa mikoa na Wilaya zote nchini,” amesema Prof. Mkumbo na kuongeza,

“Mitandao wa barabara za lami na zege (paved roads) katika mikoa umeongezeka kutoka KM 4,179 mwaka 2000 hadi Kufikia KM 11,966.38 mwaka 2023,”.

Kwamba mafanikio mengine ni pamoja na kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi kutoka vifo 760 kwa vizazi hai 100,000 mwaka 2000 hadi Kufikia vifo 104 Mwaka 2022, ikiwa tumevuka lengo la Kufikia vifo 265 ifikapo Mwaka 2025 ambapo matokeo kamili ya tathimini hii yatatolewa siku hiyo.

Ameeleza kuwa katika Mkutano huo Rais Dkt. Samia atazundua rasmi Timu Kuu ya Kitaalam ya Dira (National Vision Core Technical Team) na kamati ya usimamizi wa Dira (National Vision Streering Cmmittee), pamoja na nyenzo za kidigitali zitakazotumika katika kukusanya maoni ya Wadau.

Kwamba kwa kuwa Mkutano huo utafanyika siku ya Uhuru, Rais Dkt. Samia anatarajia kutumia siku hiyo kutoa Ujumbe Maalum katika kuadhimisha miaka 62 ya Uhuru wa Tanzania Bara.

 

Post a Comment

0 Comments