Katibu Mkuu wa Chama cha NLD, Mhe, Doyo Hassan Doyo, Amefika Katika Ofisi za Chama cha NLD na Kuchukua Fomu ya Kuomba Nafasi ya Kugombea Urais wa Jamhur ya Muungano wa Tanzania.
Katibu Mkuu wa Chama cha National League for Democracy (NLD), Doyo Hassan Doyo, leo Machi 20, 2025, ameingia katika ofisi za chama hicho na kuchukua fomu ya kugombea nafasi ya Urais katika uchaguzi mkuu ujao.
Akizungumza na waandishi wa habari, Doyo alisema kuwa endapo atapata nafasi hiyo, atajitahidi kuleta mapinduzi makubwa katika sekta mbalimbali za taifa, ikiwa ni pamoja na kuboresha sekta za afya, elimu, uchumi, na utawala. Aliongeza kuwa mabadiliko haya yatawalenga wananchi wote, na kuhakikisha kila Mtanzania anapata fursa za maendeleo.
"Kauli mbiu yetu kuelekea uchaguzi mkuu ni 'Uzalendo, Haki na Maendeleo'. Hii ni ahadi yetu kwa Watanzania, kuhakikisha tunaleta maendeleo ya kweli na kuwapa haki wananchi wote, bila ubaguzi," alisema Doyo.
Kwa upande mwingine, Doyo alisisitiza kuwa chama cha NLD kinajivunia kuwa na viongozi ambao wanajali ustawi wa wananchi na wana uwezo wa kuleta mabadiliko makubwa katika utawala na taifa hili la Tanzania. Alieleza kuwa kama atachaguliwa kuwa rais, atahakikisha nchi inaelekea kwenye mwelekeo wa kisasa, wenye mshikamano, na ambao utaleta ustawi kwa kila mwananchi mmoja, mmoja.
Chama cha NLD kinaendelea kujipanga kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa ndani ya Chama utakao fanyika April 10, 2025, huku Doyo akiongoza juhudi za kuhakikisha anapata ushindi katika nafasi hiyo ya kukiwakilisha Chama na hatimaye kuleta mabadiliko makubwa ya kisera na ya kisiasa katika uchaguzi Mkuu ujao.
By Ombe B.Kilonzo

0 Comments