DC KALLI AAHIDI UMEME WA TANESCO KUIMARISHA MRADI WA MAJI ENGARENAIBOR

NA MWANDISHI WETU, LONGIDO

Mkuu wa Wilaya ya Longido, Mhe. Salum Kalli, amewaahidi wananchi wa Kata ya Engarenaibor kuwa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) litapeleka umeme katika mradi wa maji uliopo Kijiji cha Mairowa, kwenye chanzo cha chemichemi ya Engongu, ili kuwezesha uendeshaji wa mtambo wa kusukuma maji na kuhakikisha huduma ya maji inapatikana wakati wote.

DC Kalli alitoa ahadi hiyo leo Januari 20, 2026, alipokuwa akizungumza na wananchi wa kata hiyo katika mwendelezo wa ziara yake ya kusikiliza na kutatua kero za wananchi.

Wananchi wa Engarenaibor walilalamikia tatizo la uhaba wa maji, wakibainisha kuwa chanzo kikuu cha changamoto hiyo ni ukosefu wa nishati ya uhakika ya kuendesha mtambo wa kusukuma maji.

Amesema Meneja wa TANESCO Wilaya ya Longido tayari analifanyia kazi suala hilo na amewahakikishia wananchi kuwa muda si mrefu umeme utafikishwa katika eneo la mradi huo na kuanza kutoa huduma.

“Tunalenga kuhakikisha maji yanapatikana wakati wote. Umeme utakapofikishwa kwenye chanzo hiki, mtambo utaweza kufanya kazi muda wote na wananchi watapata huduma ya uhakika ya maji safi na salama,” amesema DC Kalli.

Aidha, amesema kuwa katika jitihada za Serikali kutatua changamoto ya maji katika Kata ya Engarenaibor, Wakala wa Usambazaji wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) umepanga kutekeleza Mradi wa Maji wa Kareo katika mwaka wa fedha ujao, ambao utahusisha ujenzi wa tanki la maji lenye ujazo wa lita 50,000.

Katika hatua nyingine, DC Kalli amewahamasisha wananchi kujiunga na mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, akisema utawapunguzia gharama za matibabu na kuwawezesha kupata huduma za afya kwa urahisi popote nchini.

Ikumbukwe kuwa wakati wa kampeni, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, aliahidi kuwa ndani ya siku 100 za uongozi wake wa muhula wa pili wa Awamu ya Sita, Serikali itahakikisha kila Mtanzania anapata fursa ya kujiunga na Bima ya Afya kwa Wote.

Post a Comment

0 Comments