DC LONGIDO AAGIZA HATUA ZA HARAKA KUKOMESHA UVAMIZI WA ARDHI SOKO LA ENGARENAIBOR






NA MWANDISHI WETU, LONGIDO

Mkuu wa Wilaya ya Longido, Mhe. Salum Kalli, amemuagiza Mkuu wa Idara ya Ardhi kufika mara moja katika Kata ya Engarenaibor kushughulikia madai ya uvamizi wa eneo la Soko la Engarenaibor pamoja na ugawaji holela wa viwanja kwa baadhi ya wananchi kwa matumizi binafsi, hali inayotishia maslahi ya umma.

DC Kalli ametoa agizo hilo leo Januari 20, 2026, baada ya kusikiliza kero za wananchi wa kata hiyo waliolalamikia vitendo vya baadhi ya watu kuvamia eneo la soko, jambo linaloweza kusababisha wananchi kukosa eneo la kufanyia biashara.

Akizungumza katika mkutano huo, DC Kalli alisema:

“Kaimu Mkurugenzi yuko hapa, nenda kamweleze Mkuu wa Idara ya Ardhi aje mara moja. Wakae hapa watatue changamoto hii ya uvamizi wa soko. Tunataka kuwa na soko la kisasa. Kama kuna mtu amevamia na kuweka msingi ndani ya soko, uvunjwe.”

Ameeleza kuwa lengo la Serikali ni kuhakikisha Kata ya Engarenaibor inakuwa na soko la kisasa litakalowawezesha wananchi kufanya biashara zao kila siku na kuwa soko la mfano kwa maeneo mengine.

Aidha, DC Kalli amesema kutokana na kukua kwa kasi kwa Kata ya Engarenaibor pamoja na ongezeko la watu, kuna umuhimu wa kupanga matumizi ya ardhi kwa kuzingatia mipango miji, ikiwemo kutenga maeneo ya mitaa, barabara, soko, shule na huduma nyingine za jamii ili kuepusha ujenzi holela na kuongeza mvuto wa kimwonekano wa kata hiyo.

Katika hatua nyingine, Mkuu wa Wilaya amesema operesheni maalum itafanyika kwa lengo la kuwakamata wauzaji na watumiaji wa dawa za kulevya, ikiwemo bangi na mirungi.

Kauli hiyo imetolewa kufuatia malalamiko ya wananchi kuhusu baadhi ya vijana kujihusisha na matumizi ya bangi na mirungi hadharani, hali inayosababisha mmomonyoko wa maadili na kujiingiza katika vitendo vya kihalifu.

DC Kalli amesisitiza kuwa vitendo hivyo havikubaliki na ametangaza marufuku ya matumizi na biashara ya dawa za kulevya katika Wilaya ya Longido.

Post a Comment

0 Comments