KUELEKEA SIKU YA WANAWAKE: LONGIDO YACHOCHEA UWEZESHAJI WA KIUCHUMI NA KIJAMII










NA MWANDISHI WETU, LONGIDO

Halmashauri ya Wilaya ya Longido imegawa hati 54 za kimila za umiliki wa ardhi kwa wanawake na kutoa elimu ya ujasiriamali, uwekezaji na usawa wa kijinsia ikiwa ni maandalizi ya Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yanayoadhimishwa kila Machi 8.

Akizungumza Machi 2, 2026 wilayani humo, Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii, Bi. Grace Mghase, alisema kaulimbiu ya mwaka huu isemayo, “Haki na usawa kwa wanawake na wasichana ni msingi jumuishi kufikia Dira ya 2050,” imekuwa mwongozo wa utekelezaji wa shughuli mbalimbali zinazolenga kumwezesha mwanamke kiuchumi na kijamii.

Alisema hati hizo ziligawiwa katika vijiji vya Orbomba na Karao, hatua inayolenga kuwawezesha wanawake kumiliki rasilimali ardhi na kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo. Mbali na hilo, alibainisha kuwa wametoa elimu ya ujasiriamali na uwekezaji kwa wanawake, ikiwemo mafunzo ya kuweka akiba na kujiunga na vikundi vya VICOBA ili kupata mitaji na kukopeshana.

“Kama tunavyofahamu, wanawake ni nguzo muhimu katika jamii na familia. Hivyo, tunapomwezesha mwanamke tunaamini kuwa tumeliwezesha Taifa kwa ujumla. Kwa upande wa Halmashauri ya Wilaya ya Longido, tumekuwa tukitekeleza shughuli mbalimbali za kutoa elimu kwa wanawake. Tumetoa elimu ya ujasiriamali sambamba na utoaji wa hati za kimila za umiliki wa ardhi katika vijiji vya Karao na Orbomba, ambapo jumla ya hati 54 ziligawiwa kwa wanawake,” alisema Bi. Mghase.

Katika kukabiliana na changamoto za kijamii, Bi. Mghase alisema elimu ya usawa wa kijinsia imetolewa kwa viongozi wa kimila wa jamii ya Kimasai, kwa kuwa wana nafasi muhimu katika kupunguza vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto.

Aidha, elimu kuhusu madhara ya ukeketaji na athari zake kwa elimu ya mtoto wa kike imetolewa katika vijiji vya Orbomba na Kimokouwa.

Sambamba na hayo, Bi. Mghase alisema waliandaa bonanza la michezo lililowakutanisha wanawake watumishi, wanafunzi wa Chuo cha VETA na Longido Sekondari. Bonanza hilo lilihusisha michezo mbalimbali ikiwemo mpira wa pete, mpira wa miguu na mashindano ya kutembea na magunia, ambapo washindi walipatiwa zawadi. Lengo lilikuwa kuimarisha afya na kuhamasisha utamaduni wa michezo miongoni mwa wanawake.

Kwa kushirikiana na Dawati la Jinsia la Polisi, alisema wametoa misaada kwa wanawake wanaoishi katika mazingira magumu katika Kijiji cha Tingatinga. Vilevile, wanaendelea kutoa elimu ya msaada wa kisheria kwa makundi mbalimbali ya jamii.

Katika mwendelezo wa maadhimisho hayo, Bi. Mghase alieleza kuwa leo Machi 3, 2026 kutafanyika kongamano la wanawake wilayani humo litakalowakutanisha wanawake wa kada mbalimbali kujadili changamoto na mafanikio yao. Aidha, Machi 5, 2026 alisema watashiriki maadhimisho ya kimkoa yatakayofanyika katika Uwanja wa Ngarenaro, mkoani Arusha, kwa kupeleka vikundi vya wajasiriamali kuonesha bidhaa zao, kubadilishana mawazo na kutafuta masoko.

Aliongeza kuwa utoaji wa elimu utaendelea kwa wanafunzi wa kike katika shule za sekondari za Kamwanga na Lekule ili kuwajengea uwezo wa kujitambua, kujiamini na kufikia malengo yao.

 


Post a Comment

0 Comments