Chama Cha Mapjnduzi kimemtaka Mwenyekiti wa ACT Wazalendo, Othman Masuoud Othman, kutowapotosha Wananchi kwa kudai kuna waliojipa Mamlaka ilahali kura zilizopigwa ndizo zilizoiweka Serikali madarakani .
Kauli hiyo imetamkwa na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar,Idara ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Khamis Mbeto Khamis, aliyesema matamshi ya Mwenyekiti huyo wa ACT Wazalendo yana upungufu na walakin.
Wakati akifungua kikao cha Kamati Kuu ya ACT Wazalendo Jijini Dar es Salaam, Othman alidai kuna waliojipa Madaraka huku wakishindwa kutenda haki na kutotimiza wajibu stahiki kwa Wananchi.
Akijibu madai hayo, Mbeto alisema hakuna Serikali Duniani inayojiweka Madarakani, bila kupata ridhaa na idhini ya Wananchi kupitia ushiriki wao katika demokrasia ya Uchaguzi.
Alisema jaribio la kutaka kuiaminisha jamii na dunia ya kwamba Serikali iliojiweka madarakani, hizo ni Ngenga, Varange na sarakasi za kisiasa, jeuri na ukaidi usio na maana wala mantiki.
"Tumeshiriki Uchaguzi Mkuu Dunia nzima ikitushuhudia. Wagombea Urais, Ubunge, Uwakilishi na Udiwani wa Vyama vyote waliomba kura wakapigiwa .Chama kilichoshinda kilitangazwa na Tume ya Uchaguzi Zanzibar hivyo ni makosa kudai kuna waliojiweka Madarakani" Alisema Mbeto.
Aidha,Katibu Mwenezi huyo alisema CCM imekiita kitendo cha Othman kupita akidai mshindi amejiweka madarakani, madai hayo ni porojo na pambio zisizo na uzito wowote .
"Wenzetu kwa kutojua na kutaka
kuendekeza malumbano majukwaani wamekuwa wakibeza maendeleo bila kushirikiana
na serikali. Wananchi wapo na
wanashuhudia yaliofanyika. Kwa kubeza kwao wamejikuta wakidondoka kidemokrasia"
Alifahamisha
Hata hivyo Mbeto alimtaka Othman akubali ukweli hakuwa na nguvu za kisiasa za kumshinda mgombea Urais waCCM, ambaye tayari ameleta maendeleo yaliowaridhisha wananchi miaka mitano iliopita .
"Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 umeshafanyika na matokeo yametangazwa. Kukaa na kudhani Uchaguzi Mkuu bado haujafanyika ni kujidanganya mwenyewe. Uchaguzi umekwisha, mshindi amepatikana na ameshaunda serikali "Alisema katibu huyo Mwenezi.

0 Comments