Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
Chama cha Mapinduzi kimesema msingi wa kukubalika kwake na Wananchi si umaarufu wa jina lake, bali ni kutokana na Mikakati ya Utekelezaji wa Sera zake unaomvutia kila Mtanzania .
Aidha, CCM kimeahidi kuendelea kutumikia Wananchi kwa sababu hakuna chama cha Siasa sahihi nchini chenye uwezo , upeo na sifa za CCM.
Matamshi hayo yametamkwa na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar, Idara ya Itkadi, Uenezi na Mafunzo, Khamis Mbeto Khamisi, mara tu alipowasili Kisiwani Unguja akitokea Pemba.
Mbeto alisema Wananchi wa Tanzania kwa ujumla wao , bado wana imani kubwa kwa CCM, kutokana na uimara wa Sera zake ambazo kwa miaka yote zimesimamia Amani, Umoja na Maendeleo.
Alisema wakiwa Kisiwani Pemba, Wananchi na Wanachama wa CCM wamejitokeza kwa mamia kumlaki Naibu Katibu mkuu mpya, Abdi Mahmoud Abdi kisiwani humo.
"Ziara yetu Kisiwani Pemba imekuwa na mafanikio makubwa. Kujitokeza kwa wingi Wananchi katika mapokezi ya Naibu Katibu Mkuu wetu ni ishara ya Uhai wa chama chetu ndani ya umma" Alisema Mbeto.
Vile vile, Katibu huyo Mwenezi alisema kujitokeza huko kwa wingi kwa wananchi na mapokezi yaliotikisa ,si ishara peke yake ya kuungwa kwake mkono kwa CCM, bali ni mwanzo wa maandalizi kuelekea Mwaka 2030.
"Mila na desturi ya CCM unapomalizika Uchaguzi Mkuu mmoja huwa mwanzo wa maandalizi ya Uchaguzi Mkuu ujao. Tumeanza kujiandaa kuelekea kupata ushindi ujao. Ushindi wetu hutokana na nguvu ya Umma" Alieza.
Mbeto alisema ni makosa kwa chama cha Siasa makini kuanza kujiandaa ili kupata ushindi wa uchaguzi ujao, katika mwaka huo huo wa Uchaguzi. CCM hivyo ndivyo kinavyoishi Kisiasa" Alifafanua .
Hata hivyo , Mwenezi huyo alipoulizwa anaitazama vipi nafasi ya Wapinzani wao Kisiasa Visiwani Zanzibar, alijibu akisema inashangaza wenzao kuamua kuwa wapinga maendeleo huku CCM ikiendelea kupigania Maendeleo.
"Kupiga domo la Siasa kila uchao mabarazani bila msukumo wa Maendeleo ni kama kucheza kamari. Wananchi wanahitaji maisha bora, kuimarika kwa huduma za jamii na Uchumi mwanana "Alisisitiza .
Mbeto alisema nia ya CCM ni kufanyakazi na wenzao wa ACT Wazalendo katika Serikali ya Umoja wa kitaifa pia kushirikiana na vyama vingine vya Siasa katika nyakati zote.

0 Comments