Na Mwandishi wetu
MWENYEKITI wa Chama cha NCCR Mageuzi Ambari Haji khamisi amesema majereha walioyapata katika Uchaguzi wa Mwaka 2015 baada ya kuwa katika Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) bado hayajapona, hivyo hawapotayari kushirikiana na Chama chochote kwenye Uchaguzi wa Mwaka huu.
Ambari ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na waandishi wa habari, kuelekea chaguzi za ndani za chama hicho na Mkutano Mkuu unaotarajiwa kufanyika Aprili mwaka huu.
Amesema kuwa katika Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2015 walipoteza majimbo yao licha ya kwamba kama vyama vya UKAWA walikubaliana kuachiana maeneo lakini cha kushangaza Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Chama cha Wananchi (CUF) waliweka wagonbea wao kwenye maeneo ambayo NCCR Mageuzi walitakiwa kuachiwa wagombea wake pekee.
"Tulikubaliana Kuna baadhi ya majimbo tutaachiana lakini kilichotokea kwetu ni maumivu, tulipojiunga tulikua na majimbo manne lakini tuliporidi tumerudi na Jimbo mmoja tu"amesema Ambari.
Amesema kuwa, katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu watasimama wao wenyewe bila kushirikiana na chama chochote.
"Hatuko kwenye vyama 14 wala sita wala vyama vitatu, sisi tuko peke yetu na tutaendelea kuwa peke yetu mpaka vikao halali vya chama vitakapoona vinginevyo...kwasasa umoja tulishauvunja Dodoma kwenye mkutano mkuu.
"Hatutaki umoja kwa sababu madhara yaliyotukuta 2015 ni makubwa mpaka leo hatujapona. Tuliingia kwenye uchaguzi tukiwa na wabunge wanne tukatoka na mbunge mmoja mengine tukapoteza...sisi hatukufaidika chochote kwenye Ukawa," amesema Khamis.
Ameongeza kuwa, yako maadhimio ambayo walikubaliana na kusaini lakini vyama vingine havikuyatekeleza hivyo hawawezi kurudia makosa.
Aidha amesema kupitia mkutano mkuu utakaofanyika Aprili mwaka huu pia watatangaza jina la mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mgombea urais kwa upande wa Zanzibar pamoja na kupitisha mabadiliko ya katiba ya chama hicho.
Chama hicho kimesema kimejifunza kilipokosea na sasa kimejipanga kuhakikisha kinashiriki vizuri Uchaguzi Mkuu na kushinda kwa kishindo.

0 Comments