SERIKALI YAAGIZA WANAWAKE WANAOSOMA MASOMO YA SAYANSI WAPEWE KIPAUMBELE



*#KAZIINAONGEA* 

Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia Wizara ya Ujenzi imekitaka kitengo cha ushirikishwaji ndani ya Wizara hiyo kufuatilia wanafunzi wanaosoma masomo ya Sayansi baada ya kuhitimu kwa kuangalia na kutoa fursa mbalimbali za kuwawezesha kufikia malengo yao.

Maagizo hayo yametolewa na Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Mhandisi Balozi Aisha Amour kwa niaba ya serikali, Mha. amesisitiza pia ushirikishwaji wa Wanawake katika kazi za Barabara 

Mhandisi Aisha amesema hayo Machi 7, 2025 alipotembelea Banda la Wizara ya Ujenzi pamoja na taasisi zake, mkoani Arusha kuelekea kilele cha siku ya kimataifa ya Wanawake Machi 8 mwaka huu.

“Ni kazi ya Wizara ya Ujenzi kuhakikisha kwamba wanawake wanaosoma masomo ya Sayansi, wanafanyia kazi waliojifunza kupitia fursa mbalimbali ili kufikia malengo ambayo nchi inatarajia”- amesema Mhandisi Aisha Amour.

Aidha Mhandisi Aisha ameitaka Bodi ya Usajili wa Makandarasi (CRB) kufuatilia miradi mbalimbali inayotekelezwa na Makandarasi nchini na kuwapa mafunzo ya kufikia viwango ambavyo vitasaidia kupata miradi itakayokuwa shindanishi kwa makampuni ya nje ya nchi.

“Lengo la Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi ni kuwainua makandarasi wazawa kwa hiyo kazi ya CRB na taasisi nyingine zinazohusika na Wakandarasi ni kuhakikisha kwamba tunawatambua, kuwakuza na kuangalia namna ya kutatua changamoto zinazowakabili wakandarasi hasa wanawake kwa mafunzo na kuwapeleka kwenye miradi.”- ameongeza Mhandisi Aisha Amour.

Pia ameutaka Wakala ya Barabara Nchini (TANROADS) kuwajumuisha Makandarasi Wanawake katika miradi mikubwa ili kuona na kujifunza namna bora ya kutekeleza miradi kwa ufanisi.

*#KAZIINAONGEA*

Post a Comment

0 Comments