SHILINGI MILIONI 600 KUBORESHA BWAWA LA MAJI KISERIAN









NA ABRAHAM NTAMBARA, LONGIDO

Serikali imetenga shilingi milioni 600 kwa ajili ya kuboresha Bwawa la Kijiji cha Kiserian, ikiwa ni hatua ya kutatua changamoto ya upatikanaji wa maji katika eneo hilo.

Hayo yamebainishwa hivi karibuni na Mkuu wa Wilaya ya Longido, Mhe. Salum Kalli, wakati alipokuwa akizungumza na wananchi alipotembelea mnada wa Soko la Kiserian, Kata ya Engikaret.

“Serikali imeleta shilingi milioni 600. Tunakwenda kuboresha bwawa hili, tunataka kulifukua ili mpate maji ya uhakika. Bwawa hili litamaliza kero ya maji,” alisema Mhe. Kalli.

Aliongeza kuwa maboresho hayo yataanza hivi karibuni, huku akiwahakikishia wananchi kuwa utekelezaji wa mradi huo utafanyika kwa haraka ili kuhakikisha maji yanapatikana mapema.

Katika hatua nyingine, Mhe. Kalli alisema kuwa Serikali ina mpango wa kuboresha mnada wa Soko la Kijiji cha Kiserian kwa lengo la kuufanya ufanyike kila siku, badala ya kufanyika siku moja tu ya Ijumaa.

Alisema kuwa maboresho hayo, yakikamilika, yatawezesha wananchi kufanya biashara muda wote, kuongeza kipato chao na hivyo kuboresha maisha ya familia zao.

Mhe. Kalli alitumia pia fursa hiyo kuwapongeza wananchi kwa kushiriki uchaguzi kwa amani na kumchagua Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ushindi mkubwa wa kishindo.

Post a Comment

0 Comments