NA MWANDISHI WETU
Watumishi wa Wakala wa Usajili wa Leseni na Leseni (BRELA) wamepatiwa mafunzo maalum ya kukabiliana na majanga ya moto mahali pa kazi, yaliyotolewa na maafisa kutoka Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, kwa lengo la kuongeza usalama na utayari wa watumishi dhidi ya majanga ya moto.
Mafunzo hayo yaliyofanyika (jana) tarehe 20 Februari 2026 katika Ofisi za BRELA yalilenga kuwawezesha watumishi kutambua aina za moto, kutumia kwa usahihi vifaa vya kuzimia moto pamoja na kuchukua hatua stahiki pindi majanga yanapotokea ndani au nje ya majengo ya kazi.
Akizungumza baada ya mafumzo hayo, Afisa wa BRELA Bw. John Machela alisema mafunzo hayo yameongeza uelewa na uwezo wa vitendo katika kukabiliana na majanga ya moto siyo tu kazini bali hata majumbani.
“Mafunzo haya yametusaidia kujiandaa kikamilifu pindi changamoto za majanga ya moto zinapotokea. Yamenisaidia binafsi hata nikiwa nyumbani, kwani sasa ninaelewa namna sahihi ya kujilinda na kujiokoa,” alisema Bw. Machela.
Aidha, Bw. Machela alisisitiza kuwa elimu ya kukabiliana na majanga ya moto inapaswa kuwa endelevu na kutolewa mara kwa mara ili kuongeza ufanisi na uelewa wa watumishi li kuwakumbusha na kuwajengea uwezo zaidi.
Kwa upande wake Afisa wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji FC. Jofrey Sindika aliwakumbusha wafanyakazi wanaofanya kazi katika majengo marefu kama la BRELA kuwa ni umuhimu kutambua ramani ya jengo, njia za dharura na maeneo maalum ya mkusanyiko (assembly points) kwa ajili ya usalama zaidi.
“Ni lazima kila jengo liwe na eneo maalum la dharura kwa ajili ya mkusanyiko ili pindi tatizo linapotokea, watu waweze kukusanyika eneo hilo na kupata msaada kwa haraka,” alisema FC. Jofrey Sindika
BRELA imekuwa ikipata mafunzo hayo mara mbili kwa mwaka kwa lengo la kuimarisha uelewa na utayari wa watumishi katika kukabiliana na majanga ya moto mahali pa kazi ambapo wataalamu wa zimamoto wamekuwa wakiwakumbusha watumishi kuzingatia mafunzo wanayopata hususan katika matumizi sahihi ya vifaa vya kuzimia moto.


0 Comments