SERIKALI YAFUTA LESENI 40 ZA UTAFITI WA MADINI, sawa na Eneo la Ukubwa wa ekari 188,163




▪️Wamiliki Washindwa kuziendeleza Licha ya Kupewa Hati za Makosa

▪️Waziri Mavunde Atoa Siku 30 kwa Leseni Zingine 43 Kurekebisha Kasoro au Kufutwa

▪️Asilimia kubwa ya Leseni zinazofutwa kuelekezwa kwa makundi ya wakinamama,Vijana na wenye ulemavu

▪️Aonya uvamizi kwenye  Leseni Halali

NA MWANDISHI WETU, DODOMA

Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde ameielekeza Tume ya Madini kufuta jumla ya leseni 40 za utafiti wa madini ambao wameshindwa kuendeleza leseni hizo kwa lengo la kuimarisha usimamizi wa rasilimali za madini na kuondoa wamiliki wasiotekeleza masharti ya leseni, huku akionya kuwa Serikali haitavumilia uzembe unaokwamisha maendeleo ya Sekta ya Madini pamoja na uchumi kwa ujumla.

Waziri Mavunde ametangaza uamuzi huo leo Aprili 15, 2026 jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari, akieleza kuwa leseni hizo zimefutwa baada ya wamiliki wake kushindwa kuziendeleza licha ya kupewa hati za makosa na muda wa kurekebisha kasoro zilizobainika na kwamba zitarudishwa Serikalini kwa ajili ya  kuweka utaratibu wa kugawa kwa wachimbaji wadogo,wawekezaji walio na utayari na makundi ya Wanawake na Vijana kupitia Programu ya Mining for A Brighter Tomorrow-MBT. 

Amesema kuwa, tathmini ya kina iliyofanywa na Wizara ya Madini imeonesha uwepo wa ukiukwaji mkubwa wa masharti ya leseni, ikiwemo baadhi ya wamiliki kuhodhi maeneo bila kuyaendeleza, kushindwa kulipa ada stahiki, kutotekeleza wajibu wa ushirikishwaji wa Watanzania (Local Content), pamoja na kushindwa kutekeleza miradi ya uwajibikaji kwa jamii (CSR).

“Wapo waliokuwa wanamiliki leseni lakini hawafanyi uwekezaji wowote unaoonekana, wala kuthibitisha matumizi ya fedha katika kuendeleza maeneo yao. Hali hii hairuhusiwi kuendelea,” amesema Mavunde. 

Kwa mujibu wa Waziri Mavunde, vitendo vya kuhodhi leseni vimekuwa chanzo kikubwa cha migogoro na kuchochea uchimbaji holela, hali inayohatarisha usalama wa wananchi, mazingira na mapato ya Serikali.

“Hizi leseni 40 ni sawa na eneo lenye ukubwa wa kilomita za mraba 900 sawa na  hekari  188,163” amesisitiza Mavunde.

Katika hatua nyingine, Serikali kupitia Tume ya Madini imetoa hati za makosa kwa leseni nyingine 43, zikiwemo leseni 40 za utafutaji na tatu za uchimbaji wa kati, huku wamiliki wake wakitakiwa kurekebisha kasoro ndani ya siku 30.

Waziri Mavunde amesisitiza kuwa endapo masharti hayo hayatatekelezwa ndani ya muda uliowekwa, leseni hizo zitafutwa na maeneo husika kutolewa kwa wawekezaji wengine wenye uwezo wa kuyaendeleza. 

Akizungumzia mwenendo wa matukio ya mlipuko wa maeneo yenye madini ya dhahabu “gold rush” katika maeneo mbalimbali nchini, Waziri Mavunde ametoa onyo kali kwa watu wanaovamia maeneo yenye leseni halali wakidai kufuata taarifa za uwepo wa madini.

Ameeleza kuwa uchimbaji wowote bila leseni ni kinyume cha sheria na hautavumiliwa, akibainisha kuwa vitendo hivyo vimesababisha migogoro kati ya wachimbaji na wamiliki halali, pamoja na uharibifu wa mazingira na hatari za kiafya.

Waziri Mavunde amebainisha kuwa Serikali imeweka mikakati madhubuti ya kukabiliana na hali hiyo, ikiwemo, kudhibiti usalama wa wananchi na mali zao, kuzuia migogoro ya kimiliki, kulinda mazingira dhidi ya uchimbaji holela pamoja na kudhibiti milipuko ya magonjwa katika maeneo yenye msongamano mkubwa wa wachimbaji.

Aidha, Waziri Mavunde amekemea tabia inayoongezeka ya baadhi ya wachimbaji wadogo kuvamia maeneo yenye leseni halali, akieleza kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wote watakaokiuka sheria.

“Kuanzia sasa ni marufuku kuvamia maeneo ya leseni kwa sababu yoyote ile. Serikali haitasita kuwachukulia hatua kali wote watakaohusika,” amesisitiza Waziri Mavunde.

Hatua ya kufuta leseni 40 inaashiria msimamo thabiti wa Serikali wa kuendeleza Sekta ya Madini dhidi ya uzembe na vitendo visivyo halali, huku ikifungua ukurasa mpya wa uwajibikaji na ushindani wa haki katika matumizi ya rasilimali za taifa.

Post a Comment

0 Comments