MAFANIKIO YA BRELA KWA MWAKA WA FEDHA 2025/2026 NA MATARIJIO YA WAKALA KWA MWAKA 2026/2027



NA MWANDISHI WETU

Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) imezidi kujipambanua kama muhimili na nguzo madhubuti katika kuchochea ukuaji wa uchumi wa taifa, kupitia mikakati yake endelevu inayolenga kurasimisha shughuli za kiuchumi na kuhakikisha kuwa hakuna Mtanzania anayeachwa nyuma katika upatikanaji wa huduma za sajili na leseni. Hayo yamebainishwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Bw. Godfrey Nyaisa, wakati akifungua kikao kazi cha wafanyakazi wa Wakala hiyo kilichofanyika mkoani Morogoro tarehe 20 Juni 2026.

“Katika mwaka wa fedha wa 2025/2026, BRELA imefanikiwa kuvuka malengo na kutekeleza majukumu yake ya msingi kwa ufanisi mkubwa ikijikita katika kuboresha huduma kwa wadau, kuimarisha mifumo ya kidijitali, na kupanua wigo wa urasimishaji biashara nchini licha ya changamoto mbalimbali za kimazingira na kiuchumi zilizojitokeza” Alisema Bw. Nyaisa

Aidha, Kaimu Meneja wa Sehemu ya Mipango, Utafiti na Ubunifu wa BRELA, Bi. Alinda Lema, alibainisha kuwa mafanikio hayo yamepatikana kupitia usimamizi thabiti wa Mpango Mkakati wa miaka mitano wa 2021/22–2025/26. Katika kipindi cha kuanzia Julai 2025 hadi Juni 2026, mpango huo umewezesha mazingira ya biashara nchini kwa kuimarisha huduma za sajili na leseni, mifumo ya kiteknolojia, na usimamizi wa utendaji kazi wa watumishi. Huku kukiwa na ongezeko la kasi ya urasimishaji wa biashara, kuimarika kwa ulinzi wa haki miliki, na kurahisishwa kwa huduma zote zinazowafikia wadau wa sekta binafsi na ya umma.

“Kampuni zilizosajiliwa nchini zilipanda kutoka 18,541 katika mwaka wa fedha uliopita wa 2024/25 na kufikia kampuni 19,264 katika mwaka wa fedha wa 2025/26, ikiwa ni ongezeko la asilimia 4 linaloakisi kuongezeka kwa imani ya wawekezaji wa ndani na nje. Vilevile, upande wa urasimishaji wa biashara, usajili wa majina ya biashara uliongezeka kutoka majina 31,123 hadi kufikia 35,362, ikiwa ni ongezeko la asilimia 14” Alisema Bi. Lema

Kwa upande wa sekta ya viwanda na miliki ubunifu nayo haikuachwa nyuma, kwani ilionyesha ukuaji unaochochea azma ya Tanzania kuwa nchi ya viwanda na uchumi wa kati. Bi. Lema alifafanua kuwa utoaji wa leseni za viwanda uliongezeka kwa asilimia 50, kutoka leseni 435 hadi leseni 651 katika kipindi cha mwaka mmoja tu. Hali kadhalika, utoaji wa Hataza (Patents) kwa ajili ya kulinda wavumbuzi wa ndani ulishuhudia mapinduzi kwa kuongezeka kutoka hataza 30 hadi 61, ambalo ni ongezeko la asilimia 103, wakati usajili wa alama za biashara na huduma (Trade and Service marks) ukiongezeka kwa asilimia 10 kutoka sajili 3,148 hadi kufikia 3,455, hatua inayolinda alama na ubunifu wa wafanyabiashara sokoni.

 BRELA ilitekeleza zoezi la kaguzi elimishi kwa upande wa leseni katika soko kuu la kimkakati la Kariakoo jijini Dar es Salaam. Ukaguzi huu haukulenga kuadhibu, bali kuweka mazingira rafiki ya uendeshaji biashara na uwekezaji kwa kutoa elimu ya uzingatiaji wa sheria za nchi. Katika hatua nyingine ya uwazi na udhibiti wa mifumo ya kifedha, Wakala ilifanikiwa kufanya ukaguzi wa kina wa taarifa za wamiliki manufaa (Beneficial Ownership) katika mkoa wa Arusha, hatua iliyosaidia kuongeza uelewa na kupunguza makosa yaliyokuwa yanajitokeza katika mfumo wa usajili wa kampuni.

Mkakati huu wa ukaguzi ulienda sambamba na utoaji endelevu wa elimu kwa umma kuanzia Julai 2025 hadi Juni 2026, ambapo BRELA ilitumia mbinu mbalimbali za kisasa kuwafikia wananchi. Elimu kuhusu urasimishaji wa biashara, umuhimu wa leseni, na faida za kulinda miliki ubunifu ilitolewa kupitia mafunzo ya ana kwa ana, semina maalum, maonesho ya kibiashara, vipindi vya redio na televisheni, pamoja na kushiriki katika kliniki za biashara. Ushirikiano wa karibu na vyama vya wafanyabiashara nchini pia ulichangia kwa kiasi kikubwa kurahisisha ufikishaji wa ujumbe na kubadili mtazamo wa jamii kuelekea mifumo rasmi.

Sambamba na hayo, BRELA imepiga hatua baada ya kuzindua rasmi mfumo mpya na wa kisasa unaojulikana kama BRELA Online Services (BOS). Mfumo huu mpya ni mapinduzi kwani unajumuisha na kuunganisha huduma zote zilizokuwa zinatolewa kwa wateja kupitia mifumo miwili tofauti hapo awali, yaani Online Registrations System (ORS) na Tanzania National Business Portal (TNBP). Kupitia mfumo huu wa BOS, mteja sasa anaweza kupata huduma zote za usajili wa kampuni, majina ya biashara, alama za biashara na huduma, hataza, pamoja na leseni kupitia huo mmoja.

Akiangazia mipango na mustakabali wa Wakala hiyo kwa siku zijazo, Bi. Lema alisema kuwa katika kipindi kipya cha mwaka wa fedha kuanzia Julai 2026 hadi Juni 2027, BRELA imejipanga kuongeza takribani asilimia 17 ya urasimishaji biashara na kulinda ubunifu nchini. Mkakati huu utatekelezwa kwa kuzingatia misingi mikuu ya dira ya Taifa ya maendeleo 2050, Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (FYDP IV), pamoja na Mpango Mkakati mpya wa miaka mitano wa Wakala wa mwaka 2026/27–2030/31. Katika kufikia lengo hili, Wakala imejipanga kusajili kampuni mpya 24,103, majina ya biashara 40,460, alama za biashara na huduma 4,500, na hataza 40, huku ikipanga kutoa leseni za biashara 29,533 na leseni za viwanda 638.

Bi. Lema alisisitiza kuwa ili kuhakikisha azma hiyo inafikiwa na mazingira ya uwekezaji yanazidi kuwa ya ushindani kikanda na kimataifa, BRELA itafanya mapitio ya sheria na kanuni zote za sajili na leseni. Mapitio haya yatafanyika ili kuhakikisha sheria hizo zinaendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia duniani, kukidhi mahitaji ya sasa ya wadau, na kuendana na misingi ya uchumi wa kisasa, na hivyo kuifanya Tanzania kuwa kitovu bora zaidi cha uwekezaji na ukuaji wa biashara barani Afrika.

Post a Comment

0 Comments