Na Mwandishi Wetu , Zanzibar
Chama Cha Mapinduzi kimesikitishwa na kauli iliotolewa na Mwenyekiti wa ACT Wazalendo, Othman Masoud Othmam, kwa kutaja baadhi ya ajenda za vikao ,hatua ambayo inaweza kuathiri mustakbali wa nia njema ya pamoja.
CCM pia kimezitaka pande zote kuelewa kuwa,kila mmoja ana wajibu wa kulinda na kutunza siri za vikao,kanuni, maadili na miiko bila kuzungumzia ajenda ambazo hazija jadiliwa .
Hayo yametamkwa na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar, Idara ya Itikadi Uenezi na Mafunzo ,Khamis Mbeto Khamis, aliyesema si vyema kwa CCM au kwa ACT kuanza kutaja ajenda za vikao vya siri hadharani.
Mbeto alisema hadi sasa kilichosainiwa ni kabrasha la tamko la pamoja kuelekea kuanza mjadala wa ajenda zote zinazotakiwa kujadiliwa kwa usiri baada ya kamati ya pamoja kuundwa na kuanza kazi kwa mujibu wa hadidu za rejea.
Alisema ni muhimu sana kwa pande zote zikaficha siri za Vikao bila kutamka hadharani kabla ya kufikiwa kwa maazimio ya Kamati ya pamoja .
"Ni lazima Viongozi wa pande zote mbili wawe na kaba ya usiri unaozingatia miiko na maadili yaliokubaliwa.Upande wowote unapokiuka rejea za makubaliano kunaweza kudhoofisha njia safi na dhamira njema "Alisema Mbeto .
Aidha, Katibu huyo Mwenezi, alisema ni muhimu kila upande ukatambua kutakuwa na wajumbe wa Kamati ya pamoja ambayo ndio itakayokabidhiwa ajenda za majadiliano.
Mbeto amemtaja Mwemyekiti wa ACT Wazalendo, Othman, kwa kutaja baadhi ya ajenda ambazo bado ni siri na zitakazojadiliwa na Kamati ya pamoja baada ya makubaliano ya pamoja ya pande zote mbili kufikiwa.
Mbeto aliedai katika mkutano na Wanachama wa ACT Wazalendo uliofanyika katika , Ukumbi wa mpiga dili wilaya ya magharib B mkoa wa mjini kijiji cha kombeni, mwenyekiti wa chama hicho alikosea kutaja ajenda za vikao kana kwamba maamuzi hayo ndiyo yaliofikiwa.
"Tamko la pamoja si uamuzi wala matakwa ya upande mmoja. Jambo hili ifahamike ni nyeti lililobeba matumaini ya Wananchi.Si tangazo linaloweza kutaangazwa na chama kimoja kiushabiki" Alisisitiza Mwenezi huyo.
Mbeto alisema ikiwa Viongozi wa pande mbili za kisiasa zitaacha ushabiki au kuligeuza tamko la pamoja ni mradi wa kisiasa, haitahesabika huo kama ni uamuzi wenye mantiki na mashiko.
"Kimsingi ndio kwanza sanduku la juhudi na Urithi wa mazungumzo ya takriban miezi minane iliopita hata ukurasa wa kwanza haujafunguliwa . Uzuri wa usomaji wa kitabu kichochote msomaji anatakiwa awe na umakini na mtulivu"Alieleza Mwenezi huyo.

0 Comments