PURA YASISITIZA UWEKEZAJI NA USIMAMIZI MADHUBUTI WA SEKTA YA MAFUTA NA GESI


NA MWANDISHI WETU

Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) imesisitiza umuhimu wa kuendelea kuvutia uwekezaji, kuimarisha ushirikiano na wadau mbalimbali pamoja na kutumia ipasavyo fursa zilizopo katika sekta ya mafuta na gesi asilia ili kuongeza mchango wake katika maendeleo ya uchumi wa Taifa.

Akizungumza katika Kongamano la Siku ya Nishati (Energy Day) linaloendelea katika Ukumbi wa Mwandoro, Viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere – Sabasaba, jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa PURA, Mhandisi Charles Sangweni, alisema usimamizi na udhibiti madhubuti wa shughuli za mkondo wa juu wa petroli ni msingi muhimu wa kuhakikisha rasilimali za mafuta na gesi zinatumika kwa manufaa ya Taifa.

Mhandisi Sangweni alieleza kuwa sekta ya mafuta na gesi asilia ina nafasi kubwa katika kuchangia ukuaji wa uchumi wa Taifa kupitia uwekezaji, uendelezaji wa rasilimali na kuongeza thamani ya shughuli za kiuchumi zinazotokana na sekta hiyo.

Aliongeza kuwa ushirikiano kati ya Serikali, wawekezaji na wadau wengine wa sekta hiyo utaendelea kuwa nguzo muhimu katika kufanikisha maendeleo endelevu ya sekta ya mafuta na gesi nchini.

Kongamano hilo limewakutanisha viongozi, wataalamu, wawekezaji, washirika wa maendeleo na wadau wengine wa sekta ya nishati kujadili mwelekeo wa sekta, fursa za uwekezaji, ubunifu na matumizi ya teknolojia kwa ajili ya kuharakisha maendeleo ya Tanzania.


Post a Comment

0 Comments