Na Mwandishi Wetu, Zanzibar
Chama Cha Mapinduzi kimewataka Wafanyabiashara kwenye Masoko kuacha kupandisha bei za bidhaa za Vyakula kiholela katika Mwezi huu Mtukufufu wa Ramadhan Visiwani Zanzibar.
CCM imewanasihi Wafanyabiashara wenye tabia hiyo kutowakomoa walaji kwani si kitendo cha kiungwana .
Ushauri huo umetolewa na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar , Idara ya Itikadi, Uenezi na Mafunzo Khamis Mbeto Khamis baada ya kutembelea Masoko kadhaa katika Kisiwa cha Unguja.
Mbeto alitoa matamshi hayo alipotembelea na kujionea bei za bidhaa za Vyakula na mafuta ya kula kwenye baadhi ya Masokona kuwashauri watoa huduma hizo kupandisha bei kwa walaji si jambo jema.
Alisema Wafanyabiashara wanatakiwa kufikiria maslahi ya walaji hivyo kitendo cha kupandisha bei kiholela kwa nia ya kutaka kupata faida kubwa hakionyeshi utu na ubinadamu.
"Nimetembelea baadhi ya Masoko kadhaa nimekuta baadhi ya bidhaa hazijawasili toka maeneo mbalimbali ya nchi yetu . Kitendo cha kupandisha bei katika Mwezi huu Mtukufu hakikubaliki" Alisema Mbeto
Aidha Katibu Mwenezi huyo alisema pamoja na baadhi ya bidhaa za vyakula kutoka nje ya Zanzibar kutofika sokoni katika siku za Ramadhan za mwanzoni , kupandisha bei ni kuwaumiza walaji .
'Lazima Wafanyabiashara na Waagizaji wetu watambue kupandisha bei kubwa bila kujali wenzao ni ukatili. Biashara ziongozwe na utu na huruma kwa kuwafikiria walaji "Alieleza .
Aidha, Mbeto aliwataka watu wanaouza bidhaa kwenye Masoko, kupunguza ukali wa maneno na utani usiopendezesha katika jamii wakati huu na Mwezi Mtukufu wa Ramadhan.
" Zanzibar inasifika duniani kwa watu wake kuwa na huruma , ukarimu na uungwana wa watu wake .Utani na masihara yanayopitiliza kwa baadhi ya watu kutoa maneno makali kwenye Masoko si jambo zuri "Alisisitiza .
Hata hivyo Katibu huyo Mwenezi alihimiza na kuwashauri Watendaji dhamana wa Idara za biashara za SMZ kufuatilia kwa karibu bei za vyakula katika Masoko ya Unguja na Pemba.

0 Comments