Mhe. Salome awahimiza Wanawake kuchangamkia fursa za Nishati Safi ya Kupikia





*Sh. bilioni 3 zatengwa kwa ajili ya ruzuku kwa wajasiriamali vijana, wanawake na watu wenye mahitaji maalum

NA MWANDISHI WETU

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amewahimiza wanawake na vijana nchini  kutumia fursa zilizopo katika sekta ya nishati safi ya kupikia ili kujiimarisha kiuchumi na kuchangia maendeleo ya taifa.

Mhe. Salome amesema hayo wakati akishiriki harambee ya kutunisha mfuko wa Kikundi cha Wanawake na Mwalimu Nyerere  jijini Dodoma.

Ameeleza kuwa katika maeneo mengi ya vijijini matumizi ya nishati safi ya kupikia  bado ni madogo, jambo linalotoa nafasi kwa wananchi kushiriki katika utoaji wa elimu, ubunifu wa teknolojia na uzalishaji wa bidhaa za nishati safi ikiwemo mkaa mbadala.

“Nitoe wito kwa kikundi chenu kuangalia kwa makini eneo hili na kutumia fursa zilizopo ili kuinua uchumi wa wanachama  pamoja na kuchangia jitihada za Serikali za kulinda mazingira,” amesema.Mhe. Salome

Katika kuendeleza juhudi za kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia, Mhe. Salome  amesema Serikali kupitia Wizara ya Nishati imetenga Shilingi bilioni 10 katika mwaka wa fedha 2026/2027 ambazo zitatumika kuendesha tafiti, kukuza ubunifu wa teknolojia zinazohusiana na nishati safi ya kupikia, kutoa elimu kwa makundi mbalimbali ya jamii na kuimarisha ushirikiano na sekta binafsi.

Ameongeza kuwa, Serikali pia imetenga  Shilingi bilioni 3 kwa ajili ya kutoa ruzuku kwa wajasiriamali vijana, wanawake na watu wenye mahitaji maalum ili kuwasaidia kuzalisha mkaa mbadala na majiko banifu.

Amesisitiza kuwa fedha hizo ni fursa muhimu kwa vijana wa kike na wa kiume pamoja na makundi yenye mahitaji maalum  kujipanga katika vikundi ili kunufaika na programu hizo, kujikwamua kiuchumi na wakati huo huo kuchangia kuimarisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.

Vilevile, Mhe. Salome amesema matumizi ya nishati safi ya kupikia ni ajenda muhimu ya kitaifa inayotekelezwa chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye ameendelea kuwa kinara wa kuhamasisha matumizi ya nishati hiyo  barani Afrika na duniani.

Amesema Serikali imejiwekea lengo la kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2034 angalau asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi  katika shughuli za  kupika  ambapo kwa  sasa takwimu zinaonesha kuwa asilimia 28.6 ya Watanzania ndio wanatumia nishati safi ya kupikia.

Post a Comment

0 Comments